HOTUBA YA RAIS MAGUFULI AKIWA BUTIAMA - 06/09/2018
Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 06 Septemba, 2018 ameendelea na ziara yake Mkoani Mara ambapo amezindua mradi wa ufugaji wa samaki kwa kutumia mabwawa na vizimba Mjini Musoma na kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya lami ya Makutano – Natta (Sanzate).
Akiwa Butiama Mhe. Rais Magufuli ameongozana na Mke wa Baba wa Taifa Mama Maria Nyerere kuweka jiwe la msingi katika ujenzi wa barabara ya lami ya Makutano - Natta (Sanzate) yenye urefu wa kilometa 50 na ambayo ujenzi wake utagharimu shilingi Bilioni 54.6.
Akizungumza na wananchi wa Butiama katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Mwenge Kijijini Butiama Rais Magufuli amewahakikishia wananchi hao kuwa pamoja na kujenga barabara hiyo Serikali itaendelea kujenga barabara nyingine za kuunganisha Butiama, Mugumu na Tarime ili kuimarisha mawasilino na kuipa heshima Butiama na Mkoa mzima wa Mara ambako ndiko alikozaliwa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere.
Rais Magufuli amemshukuru Mama Maria Nyerere na familia yote kwa mchango mkubwa uliotolewa na Hayati Baba wa Taifa katika kupigania uhuru, kujenga Taifa, kupigania ukombozi wa Mataifa mengi ya Afrika na kuipatia Tanzania heshima kubwa duniani, na ameahidi kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha tatizo la maji lililopo Butiama linatatuliwa haraka iwezekanavyo.
“Nakupongeza Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa kwa kuwa na mpango wa kuleta maji Butiama, nitafuatilia, haiwezekani mahali alipozaliwa Baba wa Taifa pakakosa maji, na wewe Waziri wa TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo hakikisha hospitali ya Butiama inaboreshwa haraka na nimeagiza ile shule ya msingi Mwisenge pale Musoma Mjini aliyosoma Baba wa Taifa inajengewa uzio na majengo yake yanaboreshwa” amesisitiza Rais Magufuli.